Mbeya City yajipiga kifua dhidi ya Simba SC kubaki Ligi Kuu

By Nebart Msokwa , Nipashe
Published at 05:22 PM Jun 15 2026
Ofisa Habari wa Mbeya City, Gwamaka Mwankota.
Picha:Mpigapicha Wetu
Ofisa Habari wa Mbeya City, Gwamaka Mwankota.

Timu ya Mbeya City, imetamba kuwa itavuna alama tatu katika mchezo wa ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya kikosi Simba Sc ya jijini Dar es salaam kwenye mchezo unaotarajiwa kuchezwa kesho kutwa katika Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini hapa.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya mchezo huo, Ofisa Habari wa Mbeya City, Gwamaka Mwankota amesema kikosi cha timu hiyo kimejiandaa kuvuna alama tatu kwenye kila mchezo uliobakia ili kujinusuru na wimbi la kushuka daraja.

Amesema pamoja na timu hiyo kuonekana kuwa ipo kwenye hatari ya kushuka daraja, wao wamejipanga kuhakikisha wanasalia kwenye ligi bila kufika hatua ya mtoano.

Amekiri kuwa mchezo wao na Simba utakuwa mgumu kutokana na timu zote mbili kuwa na mahitaji ya alama tatu kwa maelezo kuwa wao wanakwepa kushuka daraja huku Simba wakihitaji ubingwa ambao mpaka sasa unashikiliwa na Yanga Sc.

“Wachezaji wetu, benchi la ufundi na menejimeti tumejiandaa kwa ajili ya kuvuna alama zote kwenye mchezo huo, sasa tunawaalika mashabiki wetu waje kuanikiza ushindi huo,” amesema Mwankota.

Amesema mbali na mchezo huo, michezo mingine waliyobakiwa nayo ni dhidi ya Dodoma Jiji, Pamba Jiji ya Mwanza na TRA United ya jijini Arusha ambayo ameeleza kuwa wakishinda yote watasalia kwenye ligi kuu.