Serikali yawanyooshea kidole wabadhilifu vyama vya ushirika

By Renatha Msungu , Nipashe
Published at 09:51 AM Jul 08 2026
Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde.
Picha: Mpigapicha Wetu
Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde.

Serikali imesema haitavumilia ubadhilifu na matumizi mabaya ya rasilimali katika vyama vya ushirika, ikisisitiza kuwa viongozi wote watakaobainika kuhusika na vitendo hivyo watachukuliwa hatua za kisheria.

 Hayo yamebainishwa  jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani yaliyowakutanisha viongozi na wanachama kutoka mikoa mbalimbali nchini.

Silinde amesema wapo baadhi ya watu wanaojiunga na vyama vya ushirika kwa lengo la kutumia vibaya fedha za wanachama, akisisitiza kuwa serikali imejipanga kuwadhibiti wote watakaobainika kufanya ubadhilifu ili kulinda maslahi ya wanaushirika.

"Serikali itaendelea kuimarisha mfumo wa ukaguzi wa mara kwa mara katika vyama vya ushirika ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na kuhakikisha wakulima wanapata manufaa stahiki kupitia shughuli za ushirika,"amesema Silinde.

Amesema dhamira ya serikali ni kujenga vyama vya ushirika imara vinavyoongeza thamani ya mazao, kuwawezesha wakulima kupata masoko na bei nzuri kupitia mifumo ya kidijitali, pamoja na kuongeza ushindani wa mazao ya Tanzania katika soko la kimataifa.

Amesema changamoto zote zilizowasilishwa na wanaushirika zinaendelea kufanyiwa kazi na serikali, huku akieleza kuwa maamuzi yenye tija yana mchango mkubwa katika kukuza sekta hiyo na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Amesema waajiri na wakurugenzi wanaodaiwa fedha za vyama vya akiba na mikopo (SACCOS) wanapaswa kulipa madeni hayo kwa wakati, akibainisha kuwa ucheleweshaji wa malipo unadhoofisha uwezo wa vyama hivyo kuwahudumia wanachama wake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC), Tito Haule, amesema sekta ya ushirika bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwamo mifumo ya kodi na upatikanaji wa mitaji, hali inayozuia ukuaji wa vyama na maendeleo ya wanachama.

Haule amesema shirikisho hilo limeiomba serikali kufanya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Ushirika ya mwaka 2002 pamoja na kuongeza mtaji wa mfuko huo, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuimarisha uzalishaji, masoko na ubora wa mazao ya kimkakati.