Vodacom yaonyesha dhamira kulinda taarifa binafsi za wateja

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 02:57 PM Jul 03 2026
Mkurugenzi wa sheria wa Vodacom Tanzania PLC Olaf Mumburi (wa pili kulia), akizungumza wakati wa mkutano wa kwanza wa mwaka wa Ulinzi wa Faragha na Taarifa Binafsi, akiwa mmoja wa wazungumzaji katika majadiliano kuhusu ulinzi wa taarifa za kifedha
Picha: Mpigapicha Wetu
Mkurugenzi wa sheria wa Vodacom Tanzania PLC Olaf Mumburi (wa pili kulia), akizungumza wakati wa mkutano wa kwanza wa mwaka wa Ulinzi wa Faragha na Taarifa Binafsi, akiwa mmoja wa wazungumzaji katika majadiliano kuhusu ulinzi wa taarifa za kifedha

Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania PLC imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi za wateja na kuchangia ujenzi wa uchumi wa kidijitali unaoaminika kupitia ushiriki wake katika Mkutano wa Kwanza wa Mwaka wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi uliofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Juni 29 hadi Julai 1, 2026.

Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania PLC imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi za wateja na kuchangia ujenzi wa uchumi wa kidijitali unaoaminika kupitia ushiriki wake katika Mkutano wa Kwanza wa Mwaka wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi uliofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Juni 29 hadi Julai 1, 2026.

Mbali na kuwa mmoja wa wadhamini wakuu wa mkutano huo ulioandaliwa na Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), Vodacom ilitambuliwa kwa mchango wake katika kuendeleza ajenda ya ulinzi wa taarifa nchini kwa kutunukiwa tuzo maalumu ya udhamini.

Tuzo hiyo ilipokelewa na Mtaalamu Mwandamizi wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Vodacom Tanzania PLC, Upendo Haji, kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa kampuni hiyo katika kufanikisha mkutano huo na kuhamasisha uelewa wa masuala ya ulinzi wa taarifa binafsi nchini.

Mkutano huo uliendeshwa kwa kaulimbiu isemayo, "Ulinzi wa Taarifa Binafsi kama Nguzo ya Kujenga Mustakabali wa Kidijitali Jumuishi kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," ikisisitiza umuhimu wa kulinda taarifa binafsi kama msingi wa kujenga uchumi wa kidijitali ulio salama, jumuishi na unaoaminika.

Kaulimbiu hiyo ilieleza kuwa kadri matumizi ya teknolojia na huduma za kidijitali yanavyoendelea kuongezeka, ndivyo ilivyo muhimu zaidi kwa taasisi za umma na binafsi kuimarisha mifumo ya ulinzi wa taarifa, kujenga imani kwa watumiaji na kuweka mazingira yanayochochea ubunifu unaowajibika.

Katika kipindi chote cha mkutano huo, viongozi waandamizi wa Vodacom walishiriki kama wazungumzaji wakuu, wakitoa uzoefu na mapendekezo kuhusu namna ya kuimarisha usimamizi wa taarifa binafsi katika mazingira ya uchumi unaozidi kutegemea teknolojia za kidijitali.

Mkurugenzi wa Udhibiti wa Hatari na Utii wa Sheria wa Vodacom Tanzania PLC, Olaf Mumburi, alishiriki katika mdahalo uliojadili ulinzi wa taarifa za kifedha na nafasi yake katika kuimarisha uchumi wa kidijitali. Alisisitiza umuhimu wa mifumo madhubuti ya usimamizi wa taarifa katika kujenga imani kwa watumiaji wa huduma za kidijitali na kuhakikisha ukuaji endelevu wa huduma za kifedha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Idara ya Taarifa Binafsi wa Vodacom Group kutoka Afrika Kusini, David Smuts, aliwasilisha mada kuhusu nafasi ya kimkakati ya Maafisa wa Ulinzi wa Taarifa (DPOs) katika kuimarisha uwajibikaji wa taasisi na kujenga imani katika uchumi wa kidijitali. Alieleza kuwa maafisa hao si wasimamizi wa uzingatiaji wa sheria pekee, bali ni nguzo muhimu katika kuhakikisha taasisi zinatumia taarifa za watu kwa uwajibikaji, uwazi na kwa kuzingatia haki za wateja.

Naye Mkuu wa Idara ya Usalama wa Mtandao wa Vodacom Tanzania PLC, Joel Kazoba, alichangia mjadala uliojadili iwapo ubunifu unaweza kustawi bila kuhatarisha faragha. Alisisitiza kuwa maendeleo ya teknolojia na ubunifu yanapaswa kwenda sambamba na ulinzi wa taarifa binafsi, huku akieleza kuwa uaminifu wa wateja hujengwa kupitia mifumo salama ya usimamizi wa taarifa pamoja na uwazi katika matumizi yake.

Mkutano huo uliwakutanisha wadhibiti wa sekta, viongozi wa taasisi za kifedha, wataalamu wa sheria, wataalamu wa teknolojia na watunga sera kutoka Tanzania na nchi nyingine za Afrika kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mifumo ya ulinzi wa taarifa binafsi katika zama za mageuzi ya kidijitali.

Kupitia ushiriki wake wa kiwango cha juu na mchango wake katika mijadala mbalimbali, Vodacom Tanzania imeendelea kuonesha kuwa ulinzi wa taarifa binafsi ni sehemu muhimu ya mkakati wake wa biashara na utoaji wa huduma kwa wateja.

Aidha, kutunukiwa tuzo ya udhamini katika mkutano huo kunathibitisha nafasi ya kampuni hiyo kama mmoja wa wadau wanaoongoza katika kuhamasisha matumizi salama ya teknolojia na kujenga mazingira ya kidijitali yenye kuaminika nchini Tanzania.