TMX yauza mazao na madini ya trilioni 6.2/-

By Yasmine Protace , Nipashe
Published at 07:10 PM Jul 03 2026
Afisa Mwandamizi wa TEHAMA wa TMX, Goodluck Luhanjo.
Picha: Mpigapicha Wetu
Afisa Mwandamizi wa TEHAMA wa TMX, Goodluck Luhanjo.

Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) limesema limefanikiwa kuuza zaidi ya tani milioni 2.165 za mazao na madini zenye thamani ya zaidi ya Sh trilioni 6.2 kupitia mfumo wake wa minada ya kidijitali tangu mwaka 2019 hadi 2026.

Hayo yamesemwa na Afisa Mwandamizi wa TEHAMA wa TMX, Goodluck Luhanjo, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Luhanjo amesema TMX imefanikiwa kuendesha minada ya kidijitali kwa mazao tisa ya kilimo pamoja na madini ya vito, huku ikiwaunganisha wadau wa sekta za kilimo, madini na mifugo kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali na wizara zinazohusika.

"Tangu mwaka 2019 hadi 2026, TMX imeuza zaidi ya tani milioni 2.165 kupitia mfumo wa minada ya kidijitali. Mfumo huu umewezesha kuunganisha wadau mbalimbali na kuongeza uwazi katika biashara ya mazao na madini," amesema.

Ameeleza kuwa mazao yanayouzwa kupitia mfumo huo ni pamoja na korosho, ufuta, mbaazi, dengu, kakao, kahawa, chai, maharage ya soya na mazao mengine ya kimkakati. Aidha, tangu mwaka 2024, TMX imeanza pia kufanya minada ya madini, ikiwemo Tanzanite, Spinel na madini mengine ya vito.

Luhanjo amesema wakati wa maonesho hayo, minada inaendelea katika mikoa ya Mtwara, Manyara, Dodoma na Morogoro, ambapo takribani tani 500 zimeuzwa kwa siku hiyo, huku bei ya juu ikiwa Sh2,410 kwa kilo.

Amesema TMX imeleta suluhisho la changamoto ya bei kwa wakulima kwa kuwawezesha kushiriki katika mfumo wa minada kupitia vyama vyao vya ushirika (AMCOS), jambo linalowawezesha kuona mchakato mzima wa mauzo kwa uwazi.

"Kupitia mfumo huu, wakulima wanaona namna wanunuzi wanavyoshindana kwa bei, idadi ya mizigo iliyoingizwa kwenye mnada na bei halisi inayopatikana. Hivyo, mnunuzi anayetoa bei nzuri zaidi ndiye anayeshinda, jambo linalomsaidia mkulima kupata thamani halisi ya mazao yake," amesema.

Amesisitiza kuwa mfumo wa minada ya kidijitali umeongeza uwazi, ushindani na ufanisi katika biashara ya mazao na madini nchini, huku ukiwawezesha wakulima na wazalishaji kupata bei zenye tija zaidi.