Tanzania yatajwa kuwa na nafasi mauzo China

By Elizabeth Zaya , Nipashe
Published at 12:55 PM Jul 05 2026
Tanzania yatajwa kuwa na nafasi mauzo China
Picha: Elizabeth Zaya
Tanzania yatajwa kuwa na nafasi mauzo China

MAKAMU wa Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara (TNCC), Boniface Ndego, amesema Tanzania ina fursa kubwa ya kuongeza mauzo ya bidhaa zake kwenda China, endapo wazalishaji wataongeza uelewa kuhusu soko la nchi hiyo pamoja na mbinu za biashara za kimataifa.

Ndego, ametoa kauli hiyo jana, wakati akizungumza katika siku ya Kliniki ya biashara ya  Ubalozi wa Tanzania nchini China iliyofanyika katika viwanja vya Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimatafa ya Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba.

Amesema katika kipindi hiki ambacho uhusiano wa kiuchumi unazidi kuimarika baina ya nchi hizo mbili, ipo haja kwa wafanyabiashara kutoka Tanzania kuongeza maarifa zaidi kuhusu fursa na soko la kimataifa.

Kwa mujibu wa Ndego, licha ya watanzania wengi kujikita katika kuagiza mashine, vifaa na bidhaa za matumizi kutoka China, bado kuna fursa kubwa ambazo hazijatumika za kuongeza mauzo ya bidhaa hususani za kilimo na bidhaa nyingine zinazozalishwa nchini kwenda katika uchumi wa pili kwa ukubwa duniani.

Ameeleza kuwa China bado ni moja ya mataifa makubwa duniani katika biashara, jambo linalofungua fursa nyingi kwa wafanyabiashara wa Tanzania wanaotafuta masoko mapya.

Amesema baadhi ya wajasiriamali bado hawana ujuzi wa kutosha kuhusu namna ya kupata wanunuzi, kufanya mazungumzo ya mikataba ya biashara, kutimiza masharti ya soko la China, na kujenga mahusiano ya biashara ya kudumu.

"Watu wengi wanafahamu jinsi ya kuagiza bidhaa kutoka China, lakini ni wachache wanaoelewa namna ya kuuza bidhaa za Tanzania katika soko hilo. Kuna haja ya kuwapa wafanyabiashara maarifa ya vitendo kuhusu biashara ya kimataifa," amesema Ndego.

Amesema kuwa kuongeza uelewa wa wajasiriamali kuhusu mazingira ya biashara nchini China kutasaidia bidhaa nyingi zaidi za Tanzania, hasa mazao ya kilimo na bidhaa zilizoongezwa thamani, kuingia katika moja ya masoko makubwa zaidi ya walaji duniani.

Kwa mujibu wake, ushirikiano kati ya Tanzania na China haupaswi kujikita tu katika uwekezaji na miundombinu, bali pia katika kujenga uwezo wa wafanyabiashara wa ndani kushiriki kwa ufanisi katika biashara ya kimataifa.

Balozi wa Tanzania nchini China, Dk. Suleiman Haji Suleiman, amesema nchi hizo zimejipanga kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu unaolenga kukuza uchumi, biashara, uwekezaji na maendeleo ya wananchi kupitia urafiki na ushirikiano wa karibu.

Amesema ushirikiano huo, ambao umejengwa kwa zaidi ya miongo kadhaa, umeendelea kuimarika kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, kuaminiana na kutanguliza maendeleo ya pande zote mbili na kwamba kupitia uhusiano huo, nchi hizo zimefanikiwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, hususani katika sekta za miundombinu, biashara, uwekezaji na teknolojia.