Tamasha la Amani kuimarisha umoja

By Marco Maduhu , Nipashe Jumapili
Published at 12:59 PM Mar 01 2026
Mbunge wa Jimbo la Kishapu, Lucy Mayenga (kushoto) akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi wakicheza drafti kwenye tamasha hilo
Picha: Marco Maduhu
Mbunge wa Jimbo la Kishapu, Lucy Mayenga (kushoto) akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi wakicheza drafti kwenye tamasha hilo

Katika jitihada za kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi, Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, imeandika historia kwa kufanikisha tamasha la amani na maendeleo, lenye lengo kuimarisha umoja kwa wananchi wilayani humo.

Tamasha hilo limefanyika jana katika shule ya Msingi Buduhe, wilayani humo.

Mgeni Rasmi katika tamasha hilo Mbunge wa Jimbo la Kishapu, Lucy Mayenga, amesema hilo ni jukwaa muhimu la kuwakutanisha wananchi wa rika na makundi mbalimbali bila kujali tofauti zao za kijamii au kisiasa, likilenga kuimarisha mshikamano, amani na kuchochea maendeleo ya wilaya.

“Nawapongeza sana wananchi wa Kishapu kwa kujitokeza kwa wingi kwenye tamasha hili, ambalo litaimarisha umoja wetu, mshikamano na kuishi kwa upendo, sababu amani ndiyo msingi wa maendeleo hivyo tuendelee kuilinda na kudumisha amani ya nchi yetu,” amesema Mayenga.

Baadhi ya washiriki wa michezo iliyofanyika katika tamasha
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi, ambaye ndiye mwandaaji wa tamasha hilo, amesema kuandaa matamasha ya michezo ni njia mojawapo ya kuwaunganisha wananchi na kuwapatia ujumbe wa serikali, ikiwamo umuhimu wa kudumisha amani na mshikamano.

Amesema michezo na burudani husaidia kuondoa tofauti miongoni mwa jamii na kujenga urafiki, hali inayochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Baadhi ya wananchi walioshiriki tamasha hilo, akiwamo Pili Mazoya, amesema limeweza kuwakutanisha watu mbalimbali na kuimarisha mshikamano na kufurahi kwa pamoja kupitia burudani ya michezo mbalimbali.

Michezo, iliyochezwa kwenye tamasha hilo ni mpira wa miguu, pete, michezo ya asili kama bao, drafti, karata, kufukuza kuku, kuvuta kamba, na mbio za baiskeli.